TAARIFA YA KAMATI YA
KUDUMU YA BUNGE YA ARDHI, MALIASILI NA MAZINGIRA KUHUSU TATHMINI YA MATATIZO
YALIYOTOKANA NA OPARESHENI TOKOMEZA ;
1.0 UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, wakati Bunge likijadili hoja ya kuahirisha shughuli za Bunge
ili kujadili jambo muhimu la dharura kwa mujibu wa Kanuni ya 47 ya Kanuni za
Kudumu za Bunge, Toleo la 2013, iliyowasilishwa na Mhe. Said Nkumba, Mbunge wa
Sikonge kuhusu Mgogoro kati ya Wafugaji na Wakulima, Hifadhi na Uwekezaji,
Mheshimiwa Spika alitoa Uamuzi ‘Speakers Ruling’ kuwa Kamati ya Ardhi,
Maliasili na Mazingira ishughulikie kazi ya kutathmini na kuangalia jinsi
Mpango wa Kupambana na Majangili ulivyopangwa na kutekelezwa na Serikali
kupitia ‘Operesheni Tokomeza’.
Kwa mujibu wa kumbukumbu za Taarifa Rasmi za Bunge za tarehe 1 Novemba 2013,
wakati Bunge likihitimisha Hoja ya Kuairisha Shughuli za Bunge, Mhe. Spika
alitoa uamuzi ufuatao:-
…Kamati ile ya kawaida ya Maliasili itaendelea na kazi yake ya kufanya tathmini
ya kuangalia jinsi mpango ule wa Kupambana na Majangili ulivyopangwa na ndani
yake itashughulikia kama kulikuwa na uzembe ama kuna watu wanahusika katika
kuondoa maisha ya watu kwa sababu za uzembe …
1.1 Kuundwa kwa Kamati Ndogo ya Uchunguzi
Mheshimiwa Spika, kufuatia uamuzi ulioutoa tarehe 01 Novemba, 2013 Kamati ya
Ardhi, Maliasili na Mazingira, ilikutana Dodoma tarehe 9 Novemba, 2013 kwa
lengo la kujadili utaratibu wa kutekeleza jukumu hilo.
Katika kikao hicho Kamati iliazimia kuunda Kamati Ndogo kwa mujibu wa Kanuni ya
117(18), ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Tole la 2013 ili iweze kushughulikia
suala hilo kikamilifu.
1.2 Hadidu za Rejea, Wajumbe wa Kamati na muda wa kazi
Mheshimiwa Spika, Kamati Ndogo ya Ardhi, Maliasili na Mazingira iliyoundwa na
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira kwa agizo lako la
tarehe 01 Novemba, 2013, ilipewa Hadidu za Rejea Nne (4) zifuatazo:-
1) Kutathmini na kuangalia jinsi Mipango ya Kupambana na Majangili
ilivyopangwa;
2) Kuangalia kasoro zilizojitokeza katika kutekeleza mpango huo;
3) Kutathmini iwapo kulikuwa na uzembe katika kutekeleza Operesheni Tokomeza
ambao ulisababisha watu wasio na hatia kupoteza maisha na mali zao; na
4) Kuchunguza migogoro ya Ardhi inayohusu Wakulima, Wafugaji na Wawekezaji
kwenye maeneo yanayozunguka hifadhi.
Mheshimiwa Spika, Kamati hii ya uchunguzi iliundwa na Wajumbe Tisa (9) kama
ifuatavyo:-
i. Mhe. James Daudi Lembeli, Mb.
ii. Mhe. Abdulkarim Esmail Shah, Mb.
iii. Mhe. Susan Limbweni Kiwanga, Mb.
iv. Mhe. Kaika Sanin’go Telele, Mb.
v. Mhe. Dk. Henry Daffa Shekifu, Mb.
vi. Mhe. Amina Andrew Clement, Mb.
vii. Mhe. Haji Khatibu Kai, Mb.
viii. Mhe. Muhammad Amour Chomboh, Mb.
ix. Mhe. Dk. Mary Mwanjelwa
Mheshimiwa Spika, Sekretarieti iliyohudumia Kamati Ndogo ya Uchunguzi iliundwa
na Wajumbe wafuatao:-
i. Ndg. Theonest K. Ruhilabake
ii. Ndg. Gerald S. Magili
iii. Ndg. Chacha T. Nyakega
iv. Ndg. Stanslaus W.Kagisa
Mheshimiwa Spika, Kamati Ndogo ya Ardhi, Maliasili na Mazingira ilitakiwa
kutekeleza majukumu yake na kuwasilisha ripoti katika Mkutano wa Kumi na Nne
(14) wa Bunge. Hivyo basi, baada ya uteuzi huo, Wajumbe wa Kamati Ndogo
walipanga kuanza kazi tarehe 25 Novemba, 2013 na kuikamilisha ifikapo tarehe 15
Desemba, 2013.
1.3 Njia zilizotumika katika kukamilisha kazi
Mheshimiwa Spika, Kamati Ndogo ya Ardhi, Maliasili na Mazingira ilitekeleza
majukumu yake kwa kuongozwa na Hadidu za Rejea ilizopewa kwa kufanya rejea na
kuzingatia yafuatayo:-
a) Kusoma na kuchambua nyaraka zilizoandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii
katika kuandaa na kutekeleza Operesheni Tokomeza nchini. Nyaraka hizo ni hizi
zifuatazo:-
i. Mpango Kazi wa Operesheni Tokomeza (Concept Paper)
ii. Tathmini ya Utekelezaji wa Operesheni Tokomeza.
iii. Sheria ya Kinga, Maadili na Madaraka ya Bunge (Na.3) 1988
iv. Sheria ya Wanyamapori (Na. 5) 2009
v. Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la mwaka 2013
b) Kufanya mahojiano na watu mbalimbali:-
i. Waziri wa Maliasili na Utalii
ii. Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii
iii. Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori
iv. Mkurugenzi Msaidizi Kikosi wa Dhidi ya Ujangili
v. Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi
vi. Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA)
vii. Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA)
viii. Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Hifadhi za Misitu (TFS)
ix. Mahojiano na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge
c) Kuzuru maeneo yaliyoanishwa katika Taarifa ya Wizara kuhusiana na
utekelezaji wa Operesheni Tokomeza na yale yenye migogoro kati ya Wakulima au
Wafugaji na Wawekezaji katika maeneo ya hifadhi kwa lengo la kuhakiki (verify)
masuala yaliyoainishwa kupitia uchambuzi uliofanywa na Kamati.
2.0 KUPOKEA NA KUCHAMBUA NYARAKA MBALIMBALI ZILIZOHUSU OPERESHENI TOKOMEZA
Mheshimiwa Spika, Hadidu Rejea ya kwanza iliitaka Kamati Ndogo ya Ardhi,
Malisili na Mazingira, kufanya tathmini na kuangalia jinsi mipango ya kupambana
na majangili ilivyopangwa. Ili kukamilisha jukumu hilo, Kamati ilifanya
yafuatayo:-
a) Kupitia na kuchambaua Mpango Kazi wa Operesheni Tokomeza (Concept Paper)
ulioandaliwa na Wizara
b) Kupitia na kuchambua Tathmini ya Utekelezaji wa Operesheni Tokomeza.
2.1 Uchambuzi kuhusu Mpango Kazi wa Operesheni Tokomeza
Mheshimiwa Spika, katika kuchambua Mpango Kazi wa Operesheni Tokomeza kwa lengo
la kupata uelewa zaidi wa namna operesheni hiyo ilivyopangwa na kutekelezwa,
Kamati ilibaini kuwa, mpango huo uliandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii
na ulikuwa na mambo yafuatayo:-
i. Ukubwa wa tatizo la ujangili
ii. Aina za ujangili na sababu za ukuaji wake
iii. Maeneo yaliyoathiriwa zaidi na ujangili
iv. Malengo ya Operesheni Tokomeza
v. Njia zilizotumika kutekeleza operesheni
vi. Maeneo ya operesheni na gharama za utekelezaji
vii. Tamko la Serikali kusitisha Operesheni Tokomeza
2.1.1 Ukubwa wa tatizo la ujangili
Mheshimiwa Spika, Kamati ilibaini kuwa, tatizo la ujangili ni kubwa na limekuwa
likisababisha idadi ya Tembo iendelee kupungua nchini. Takwimu zinaonesha kuwa,
idadi ya Tembo imepungua kutoka 350,000 (miaka ya 1970) hadi kufikia 55,000
(mwaka 1989). Juhudi za kukabiliana na hali hiyo kupitia Operesheni zilizowahi
kutekelezwa huko nyuma zilisaidia kuongeza idadi ya
Tembo hadi 141,000 (mwaka 2006) ingawa ilishuka tena hadi kufikia 110,000
(mwaka 2009).
2.1.2 Aina za ujangili na sababu za ukuaji wake
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Taarifa ya Serikali, vitendo vya ujangili
vinavyofanyika nchini vimegawanyika katika makundi mawili yafuatayo:-
i. Ujangili wa Kujikimu (subsistance poaching)
Aina hii ya ujangili inahusisha watu wenye kipato kidogo na hulenga zaidi
katika kujipatia kitoweo na fedha kwa ajili ya kukidhi mahitaji mengine. Ujangili
wa aina hii huathiri zaidi wanyama wanaoliwa na si Tembo.
ii. Ujangili wa Biashara (commercial poaching)
Aina hii ya ujangili inahusisha zaidi watu wenye uwezo mkubwa wa kifedha na
hulenga kupata nyara zenye thamani kubwa. Wanyama wanaoathiriwa zaidi na aina
hii ya ujangili ni pamoja na Tembo, Faru, Simba na Chui.
Mheshimiwa Spika, taarifa ilibainisha kuwa, kuongezeka kwa masoko haramu katika
nchi za Asia na Mashariki ya Kati ambayo yanatoa bei kubwa ya nyara hizo,
imekuwa ni chachu ya kuimarika kwa mitandao inayojihusisha na ujangili (ndani
na nje ya nchi) na hivyo kusababisha ongezeko kubwa la vitendo vya ujangili.
2.1.3 Maeneo yaliyoathiriwa zaidi na ujangili
Mheshimiwa Spika,Mpango Kazi waKupambana na Ujangili ulilenga kujikita katika
maeneo yaliyoathiriwa zaidi na ujangili wa wanyamapori na misitu. Mpango huo
ulioelezewa kuwa niwa muda mrefu na kusimamiwa na kikosi kazi cha Taifa
(national task force),umeanisha maeneo yafuatayo kuwa ndiyo yaliyoathirika
zaidi:-
i. Pori la Akiba Selous
ii. Hifadhi ya Taifa Serengeti, Pori la Akiba Maswa na Pori Tengefu la
Loliondo.
iii. Hifadhi ya Taifa Katavi na Mapori ya Akiba Rukwa na Lukwati.
iv. Hifadhi ya Taifa Mikumi
v. Hifadhi ya Ngorongoro na Hifadhi za Taifa Tarangire na Ziwa Manyara.
vi. Mapori ya Akiba Burigi, Biharamuro, Ibanda na Rumanyika.
vii. Mapori ya Akiba Moyowosi, Kimisi, Ugalla na Hifadhi ya Misitu Luganzo.
2.1.4 Malengo ya Operesheni Tokomeza
Mheshimiwa Spika, Operesheni Tokomeza ambayo ilizinduliwa rasmi tarehe 04
Oktoba, 2013 ilikuwa na malengo yafuatayo:-
i. Kuzuia vitendo vya ujangili ndani na nje ya Hifadhi za Taifa, Mapori ya
Akiba, Mapori Tengefu, Mamlaka ya Hifadhi Ngorongoro na Misitu ya Hifadhi na
kufanya operesheni maeneo yote yaliyoathiriwa na ujangili.
ii. Kuwatambua mapema majangili na kujua nyendo zao ndani na nje ya maeneo ya
hifadhi.
iii. Kuwakamata na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria wafanyabiashara haramu
wa nyara za Serikali na mazao ya misitu.
iv. Kuvunja mitandao ya wafadhili, wanunuzi wadogo na wakubwa pamoja na
mawakala wa biashara haramu ya nyara za Serikali na mazao ya misitu.
v. Kufuatilia na kukamata mali za majangili zilizotokana na biashara haramu ya
nyara za Serikali na mazao ya misitu.
2.1.5 Njia zilizotumika kutekeleza Operesheni Tokomeza
Mheshimiwa Spika, Kamati ilibaini kuwa, Mpango Kazi wa Serikali kuhusiana na
Operesheni Tokomeza, uliainisha kuwa operesheni hiyo itaendeshwa kwa kutekeleza
mambo yafuatayo:-
i. Kufanya uchambuzi wa kina wa watuhumiwa wa mtandao wa ujangili wa nyara za
Serikali na wavunaji na wasafirishaji haramu wa mazao ya misitu.
ii. Kuwakamata watuhumiwa wote waliobainishwa kwenye taarifa za kiintelijensia.
iii. Kupiga picha na kuchora ramani ya eneo la tukio kwa kila mtuhumiwa (sketch
map).
iv. Kuhoji na kuandika maelezo ya watuhumiwa wa ujangili wa nyara za Serikali
na wavunaji na wasafirishaji haramu wa mazao ya misitu.
v. Kukusanya na kuhifadhi vielelezo vyote vitakavyokamatwa kutoka kwa majangili
kwa ajili ya kujenga ushahidi mahakamani.
vi. Kuandika maelezo ya mashahidi na askari wakamataji kwa ajili ya kujenga
ushahidi mahakamani.
vii. Kuandaa mashitaka dhidi ya watuhumiwa na kuwapeleka mahakamani ili sheria
ichukue mkondo wake.
2.1.6 Maeneo ya Operesheni na gharama za utekelezaji
Mheshimiwa Spika,Mpango Kazi wa Operesheni Tokomeza ulianisha kuwepo awamu
mbili za utekelezaji ambazoni; Mpango Kazi wa Muda Mfupi na Mpango Kazi wa Muda
Mrefu.
Katika Mpango Kazi wa Muda mfupi itafanyika operesheni maalum katika maeneo
yote ya ndani na nje ya hifadhi za wanyamapori na misitu nchi nzima. Maeneo
hayo yaligawanywa katika kanda 12 za utekelezaji kama ifuatavyo:-
i. Selous, Mikumi, Udzungwa, Lukwika/ Lumesule na Liparamba,
ii. Burigi/Biharamuro, Ibanda/Rumanyika na Rubondo,
iii. Moyowosi, Ugalla na Lugazo,
iv. Serengeti, Loliondo, Maswa, Ikorongo na Kijeshi,
v. Kilimanjaro, Arusha, Mkomazi/Umba, Simanjiro na Longido,
vi. Tarangile, Manyara, Karatu/Ngorongoro, Swagaswaga na Mkungunero,
vii. Rungwa, Ruaha, Mpanda – Kipengele,
viii. Rukwa, Lukwati, Katavi, Lwafi, Piti na Wembere,
ix. Mahale na Gombe,
x. Saadani na kwenye maeneo yenye misitu ya mikoko,
xi. Pori Tengefu la Handeni, Kilindi na Mkinga na
xii. Msitu wa Kazimzumbwi, Kisarawe, Rufiji na Mkuranga,
Mheshimiwa Spika, ilianishwa kuwa, awamu ya kwanza ya Mpango Kazi wa muda mfupi
ingegharimu jumla ya Tshs. 3,968,168,667/= ambazo zingechangwa na Taasisi za
wanyamapori (WD, TANAPA, NCAA na TFS) kwa kila moja jumla ya Tshs.
992,042,167/=
2.1.7 Tamko la Serikali kusitisha Operesheni
Mheshimiwa Spika, kufuatia michango na malalamiko ya Waheshimiwa Wabunge wakati
wakichangia hoja iliyotolewa na Mhe. Said Nkumba Mbunge wa Sikonge, pamoja na
maagizo ya Bunge kutaka Serikaliitoe maelezo kuhusu hoja zilizotolewa na
Waheshimiwa Wabunge, Serikali ilitoa Tamko la kusitisha Operesheni Tokomeza
tarehe 01 Novemba, 2013.
2.2 Uchambuzi wa Taarifa ya awali ya Utekelezaji wa Operesheni Tokomeza
Mheshimiwa Spika, taarifa hii ya awali kuhusiana na utekelezaji wa Operesheni
Tokomeza ilikuwa na mambo yafuatayo:-
i. Washiriki wa operesheni
ii. Awamu za operesheni
iii. Mafanikio ya operesheni
iv. Idadi ya watuhumiwa na kesi zilizofunguliwa
v. Changamoto za operesheni
2.2.1 Washiriki wa Operesheni
Mheshimiwa Spika, Operesheni Tokomeza ilihusisha jumla ya washiriki 2,371
kutoka vyombo vya Ulinzi na Usalama kwa mgawanyo ufuatao:-
i. Wanajeshi (885) kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania,
ii. Askari (480) kutoka Jeshi la Polisi,
iii. Askari (440) kutoka Kikosi Dhidi ya Ujangili (KDU)
iv. Askari Wanyamapori (383) kutoka Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA)
v. Askari (99) kutoka Wakala wa Huduma za Misitu (TFS)
vi. Askari Wanyamapori (51) kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA)
vii. Waendesha Mashitaka (23) na
viii. Mahakimu (100)
2.2.2 Awamu za Operesheni
Mheshimiwa Spika, Operesheni Tokomeza ilipangwa kutekelezwa katika awamu Nne
(4) kama ifuatavyo:-
i. Awamu ya kwanza ambayo ililenga kusaka Silaha za Kivita na Meno ya Tembo
kutoka miongoni mwa wanaojihusisha na vitendo vya ujangili.
ii. Awamu ya pili ambayo ililenga kusaka silaha zisizomilikiwa kihalali na zile
zinazomilikiwa kihalali lakini zinasadikiwa kutumika kwenye vitendo vya
ujangili.
iii. Awamu ya tatu, ambayo ililenga kutafuta yalipo Maghala ya Nyara, kusaka
Wafadhili na Wanunuzi wa nyara hizo na kuwabaini watu wanaowakingia kifua
wahusika wa vitendo vya ujangili.
iv. Awamu ya nne, ambayo ililenga kukamata Nyara nyingine mbali na Meno ya
Tembo na kuhakikisha watu walio katika makundi yafuatayo wanakamatwa:-
- Wawindaji haramu,
- Wavunaji haramu wa mazao ya misitu,
- Watu wanaolisha Mifugo ndani ya hifadhi, na
- Watu waliojenga ndani ya maeneo ya hifadhi
2.2.3 Mafanikio ya Operesheni Tokomeza
a) Idadi ya watuhumiwa na kesi zilizofunguliwa
Mheshimiwa Spika, tangu kuanza kutekelezwa kwaOperesheni Tokomeza (tarehe 04
Oktoba, 2013 hadi ilipositishwa (tarehe 01 Novemba, 2013) jumla ya kesi 687
zilifunguliwa zikiwahusisha watuhumiwa 1,030 katika maeneo yote kama
ifuatavyo:-
i. Kanda ya Kwanza kesi 105 zikiwahusisha watuhumiwa 105
ii. Kanda ya Pili kesi 370 ambazo zilihusisha watuhumiwa 375
iii. Kanda ya Tatu kesi 165 zilizohusisha watuhumiwa 498
iv. Kanda ya Nne kesi 47 zilizohusisha watuhumiwa 52
Mheshimiwa Spika, hadi wakati Operesheni Tokomeza inasitishwa tarehe 01
Novemba, 2013 kati ya Kesi 687 zilizokuwa zimefunguliwa ni 132 tu ndiyo
zilikuwa zimetolewa maamuzi na 555 bado zilikuwa katika hatua ya kusikilizwa.
(Tazama Kiambatisho Na. 1)
i. Kukamatwa kwa meno ya Tembo 211 yenye uzito wa kilo 522, meno ya Ngiri 11,
Mikia ya wanyama mbalimbali 36, Ngozi za wanyama mbalimbali 21, Pembe za Swala
46, Mitego ya wanyama 134, ng’ombe 7,621 Baiskeli 58, Pikipiki 8 na Magari 9.
ii. Kupungua kwa kasi ya mauaji ya Tembo kutoka wastani wa Tembo wawili (2) kwa
siku hadi tembo wawili tu katika kipindi chote cha operesheni (siku 29).
iii. Hadi kufikia tarehe 11 Novemba, 2013 jumla ya Bunduki za Kijeshi 18
zilikamatwa, Bunduki za kiraia 1579, Risasi 1964, Mbao vipande 27,913, Mkaa
Magunia 1242, Magogo 858 na Misumeno 60. Vyote hivyo vilikamatwa katika Kanda
ya Nne.
2.2.4 Changamoto za Operesheni Tokomeza
a) Vifo vilivyotokea wakati wa Operesheni
Mheshimiwa Spika,Taarifa ya Serikaliiliainisha vifo kamachangamoto kubwa
iliyojitokeza wakati wautekelezaji wa Operesheni Tokomeza kutokana na watumishi
6 na watuhumiwa 13 kupoteza maisha. (Tazama Kiambatisho Na. 2)
b) Hujuma dhidi ya Operesheni
Mheshimiwa Spika, taarifa ya Serikali ilifafanua kuwa,utekelezaji wa Operesheni
Tokomeza ulikumbwa na vitendo vya hujuma kutoka kwa baadhi ya makundi ya jamii
kama ifuatavyo:-
i. Mamluki miongoni wa washiriki wa Operesheni. Mfano; kukamatwa kwa Askari
Polisi na Askari Wanyamapori wakisindikiza gari lenye Meno ya Tembo, na gari la
Serikalikutumika kusafirisha Meno ya Tembo.
ii. Vyombo vya Habari kutumika kuvuruga operesheni kwakueneza propaganda
zilizolenga kushawishi wananchi kupinga operesheni hiyo.
iii. Baadhi ya wamiliki wa silaha kutuhumiwa kutoa silaha zao ili zitumike kwa
ajili ya vitendo vya ujangili.
C) Tuhuma dhidi ya Operesheni
Mheshimiwa Spika, taarifa ya Serikai ilifafanua kuwa,ingawa lengo la operesheni
lilikuwa ni kupambana na vitendo vya ujangili dhidi ya raslimali za Taifa,
utekelezaji wake ulikumbwa na tuhuma kadhaa zikiwemo zifuatazo:-
i. Mateso dhidi ya watuhumiwa yaliyosababisha maumivu, kupata ulemavu wa kudumu
na hata wengine kupoteza maisha (Mfano; Marehemu Emiliana Gasper Maro wa
Gallapo – Babati).
ii. Matumizi mabaya ya Silaha (Mfano; Mzee wa miaka 70 kuuawa kwa kupigwa
risasi 3).
iii. Nyumba za wananchi kuchomwa moto (Mfano; Kijiji cha Kabage Wilaya ya
Mpanda – Katavi).
iv. Mifugo kuuawa kikatili kwa kuchomwa moto na kupigwa risasi (Mfano; Ng’ombe
60 kuuawa kwakupigwa risasi).
v. Kukosekana kwa mwongozo wa utoaji wa taarifa jambo lililosababisha viongozi
husika wa Serikali kutopewa taarifa muhimu za utekelezaji wa Operesheni.
(Mfano; Waziri wa Maliasili naUtalii, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Waziri
wa Ulinzi na Wakuu wa Mikoa na Wilaya).
vi. Askari waliotuhumiwa kukiuka taratibu kukataa kutoa ushirikiano wa kutosha
pale walipohitajika kufanya hivyo.
vii. Kutoshirikishwa kwa viongozi wa Mamlaka za Utawala katika ngazi za Mikoa
na Wilaya.
3.0 MAHOJIANO BAINA YA KAMATI NA WIZARA PAMOJA NA WABUNGE
Mheshimiwa Spika, Kamati ilifanya mahojiano na makundi yafuatayo:-
i. Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Taasisi zake
ii. Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
iii. Waheshimiwa Wabunge
3.1 Mahojiano baina ya Kamati na Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na
Taasisi zake
Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha wajumbe wa Kamati wanapata uelewa wa kutosha
kuhusiana na Operesheni Tokomeza, Kamati liagiza uongozi wa Wizara ya Maliasili
na Utalii ukiongozwa na Waziri, kufika mbele ya Kamati ili kueleza namna
Operesheni Tokomeza ilivyoandaliwa na kutekelezwa hadi ilipositishwa kupitia
tamko la Serikali lililotolewa Bungeni tarehe 01 Novemba, 2013.
Mheshimiwa Spika, Kamati ilikutana na Waziri wa Maliasili na Utalii pamoja na
timu yake kwa siku tatu, tarehe 28- 29 Novemba, na tarehe 01 Desemba, 2013.
Katika vikao hivyo, Waziri aliieleza Kamati juu ya Mpango Kazi wa Operesheni
Tokomeza, raslimali (watu na fedha) pamoja na tathmini iliyofanyika kwa kipindi
ambacho Operesheni Tokomeza ilitekelezwa.
Mheshimiwa Spika, katika mahojiano na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Balozi
Khamis Kagasheki, Mb na watendaji wake Kamati ilifahamishwa yafuatayo:-
i. Kwamba Operesheni Tokomeza ilikuwa ya kijeshikama alivyonukuliwa katika
Taarifa Rasmi za Bunge (Hansard) akisema: “…Operesheni ilikuwa ya kijeshi.
Ilikuwa ya kijeshi kwa sababu ilitekelezwa kwa amri ya jeshi Namba 0001/13
iliyotolewa tarehe 28 Septemba, 2013 na kusainiwa na Mkuu wa Majeshi ya
Ulinzi…”
ii. Kwamba, kinadharia inaonekana kwamba, Waziri wa Maliasili na Utalii ndiye
alikuwa Msemaji Mkuu, lakini kiuhalisia hakuwa msemaji mkuu wa Operesheni
Tokomeza kama alivyonukuliwa katika Taarifa Rasmi za Bunge akisema;
“…kinadharia inaweza ikasemekana kwamba mimi ndiye msemaji mkuu, lakini mimi
sikuwa msemaji mkuu wa Operesheni Tokomeza …”
iii. Utekelezaji wa Operesheni Tokomeza ulisimamiwa na Jeshi la Wananchi wa
Tanzania.
iv. Taarifa za mwenendo wa operesheni zilikuwa zinapelekwa moja kwa moja kwa
Mkuu wa Majeshi na kwamba, hazikumfikia Waziri wa Maliasili na Utalii.
v. Operesheni Tokomeza iliingiliwa na Wanasiasa.
vi. Pamoja na Mpango kazi huo kuandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii, kwa
namna ambayo haieleweki Waziri hakuuona wala kuidhinisha rasimu ya mwisho ya
Mpango huo. Hiyo ilidhihirika mbele ya Kamati kutokana na Waziri kukiri kwamba
hakuuona wala kuudhinisha
3.1.1 Tathmini ya Kamati kuhusu majibu ya Waziri wa Maliasili na Utalii pamoja
na watendaji wa Wizara
Mheshimiwa Spika,kwa kutumia tathmini ya awali ya nyaraka zilizowasilishwa
pamoja na mahojiano na Waziri ilionekana kwamba, Operesheni Tokomeza
iliandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kushirikiana na taasisi zilizo
chini yake na kushirikisha vyombo vya Ulinzi na Usalama.
Mheshimiwa Spika, licha Mpango wa Operesheni Tokomeza kuandaliwa na Wizara ya
Maliasili na Utalii, hata hivyo utekelezaji wake ulisimamiwa na kuongozwa na
Jeshi la Wananchi wa Tanzania.
Hatua ya jeshi kuchukua jukumu la kuongoza Operesheni Tokomeza, lilifanya
viongozi wa Wizara kujiengua katika jukumu la kuongoza (ead agency) na badala
yake kuacha jukumu hilo kwa Jeshi pekee jambo lililotafsiriwa kwamba,
Operesheni Tokomeza ilikuwa ya kijeshi.
Mheshimiwa Spika, kupitia mahojiano ilibainika kwamba, hakukuwa na utaratibu
mzuri wa kupashana habari kuhusiana na mwenendo mzima wa Operesheni Tokomeza
jambo lililofanya baadhi ya wahusika kutotambua kikamilifu wajibu waokatika
Operesheni hiyo.Mfano mzuri ni kwamba, licha ya kuelezwa kwenye Kanuni za
Utendaji (Operational Guidelines)za Operesheni Tokomeza kwamba, Waziri wa
Maliasili na Utalii ndiye atakuwa Msemaji Mkuu wa Operesheni Tokomeza, bado
Mhe. Waziri hakutekeleza jukumu hilokwani alikwishatoa mapendekezo katika
rasimu kwamba Msemaji Mkuu awe ni Mkurugenzi wa Wanyamapori.
Aidha, Kamati ilibaini kuwa baadhi ya Watendaji wa juu wa Wizara
walidaiwakukwamishautekelezaji wa maagizo ya Waziri wa Maliasili na Utalii
kutokana na kuingilia mawasiliano aliyokuwa anayafanya na baadhi ya Watumishi.
Mfano ni majibizano kwa njia ya barua pepe kati ya Waziri na Katibu Mkuu,
Waziri na Mkurugenzi wa Wanyamapori na pia Katibu Mkuu na Mkurugenzi wa
Wanyamapori. Kwa mujibu wa majibizano hayo Waziri anaonekana kushangazwa na
hatua ya Katibu Mkuu kuhoji hatua ya yeye kumuita mmoja wa mtumishi wa Wizara
ofisini kwake. (Kiambatisho Na. 3)
Mheshimiwa Spika, kukosekana kwa mfumo mzuri wa kupashana habari kwa pande
husika kuhusu mwenendo mzima wa Operesheni Tokomeza, kulionekana kuathiri
utaratibu mzima wa viongozi husika akiwemo Waziri wa Maliasili na Utalii,
kupata taarifa zinazotakiwa kwa wakati. Hali hiyo ilichangia utekelezaji wa
Operesheni Tokomeza kukumbwa na athari ambazo zingeweza kuepukika iwapo
kungekuwa na mfumo mzuri wa mawasiliano.
Mheshimiwa Spika, kupitia mahojiano pia Kamati ilibaini uwepo wa hujuma kutoka
kwa viongozi wa kisiasa na Serikali ambao kwa namna moja au nyingine
walionekana kuhusishwa na Operesheni Tokomeza ama wao binafsi au ndugu zao.
Mheshimiwa Spika, miongoni mwa hujuma ambazo Kamati ilizibaini kupitia
mahojiano naWaziri wa Maliasili na Utalii na Watendaji wake ni pamoja na:-
i. Baadhi ya watuhumiwa wenye mahusiano na viongozi wa kisiasa kutumia majina
ya viongozi hao kuingilia utekelezaji wa Operesheni Tokomeza.
ii. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kutuhumiwa kujihusisha navitendo vya ujangili
na biashara haramu ya nyara za Serikali.
iii. Baadhi ya Mawaziri kutoa kauli zenye kuingilia utekelezaji wa Operesheni
Tokomeza. (Mfano: kutoa maelekezo kwa wahusika wa Operesheni Tokomeza kwamba
wasiguse viongozi wa kisiasa wa ngazi zote).
iv. Baadhi ya viongozi wavyombo vya Ulinzi na Usalama kushiriki kudhoofisha
utekelezaji wa Operesheni Tokomeza kwa kusindikiza au kusaidia watuhumiwa wa
ujangili kutoroka. (Mfano; viongozi wa Polisi wa Wilaya na Mikoa)
Mheshimiwa Spika, kubainika kwa hujuma hizo ni ishara tosha kwamba hata ndani
ya Serikali yenyewe hakukuwa na dhamira ya dhati kwa baadhi ya kwa viongozi na
watendaji katika kuhakikisha vita dhidi ya vitendo vya kijangili inapiganwa
kikamilifu.
Hali hiyo ilisababisha utekelezaji wa operesheni kukumbwa na athari nyingi kama
vile; wananchi kupoteza maisha, mifugo kuuawa kwa kuchomwa moto, njaa, kiu au
kupigwa risasi), upotevu wa mali, nyumba kuchomwa moto na vitendo vya ukatili
dhidi ya wananchi ambavyo vilikiuka haki za kibinadamu. Hali hiyo imesababisha
utekelezaji wazoezi la Operesheni Tokomeza kutafsiriwa kwamba ulilenga wananchi
wasio na hatia na kuacha wahusika wa ujangili.
3.2 Mahojiano baina ya Kamati na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 30 Novemba, 2013 Kamati ilikutana na kufanya
mahojiano na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ili kubaini namna ilivyoshiriki
katika Operesheni Tokomeza.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Dk. Emmanuel Nchimbi, Mb alieleza kuwa,
operesheni hii ilikuwa na lengo la kutimiza azma (Commitment) ya Serikali
iliyoitoa Bungeni kwamba, inakusudia kufanya Operesheni ya kupambana na
majangili. Wizara yake ilishiriki kwa kutoa Askari Polisi 504 pamoja na baadhi
ya vyombo vya usafiri na kwamba vyombo vya Ulinzi na Usalama vya nchi vilikuwa
vikikutana mara kwa mara kwa lengo la kuandaa mkakati wa namna ya kushirikiana
katika kutekeleza mpango huo wa vita dhidi ya ujangili.
Mheshimiwa Spika,Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi alikiri kuwa, licha ya lengo
la operesheni kuwa zuri, kulijitokeza changamoto kadhaa zilizotokana na baadhi
ya washiriki wa operesheni kwenda kinyume na malengo yaliyokusudiwa kama vile;
ukatili dhidi ya mifugo na vitendo vya unyanyasaji wa wananchi kwa kuwatesa
kiasi cha kuwasababishia ulemavu wa kudumu au vifo.
Pia Mheshimiwa Waziri alikiri kwamba, kutokuwepo mfumo mzuri wa mawasiliano na
Operesheni kuongozwa na jeshi, iliashiria kwamba taarifa za operesheni zilikuwa
zinakwenda kwa Mkuu wa Majeshi – CDF moja kwa moja na hivyo kufanya pande
zingine zinazohusika zisijue kinachoendelea.
3.2.1 Tathmini ya Kamati kuhusu majibu ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na
watendaji wake
Mheshimiwa Spika, Kamati ilibaini kuwepo kwamawasiliano hafifu kati ya Wizara
ya Maliasili na Utalii na Wizara nyingine zilizoshiriki katika operesheni
hii.Pia,kukosekana kwa mfumo mzuri wa mawasiliano, kuliikosesha Wizara ya
Maliasili na Utalii ambayo iliandaa na kugharamia Operesheni Tokomeza,fursa
ambazo zingeiwezesha kufanya tathmini kuhusu utekelezaji wa Operesheni hii.
Aidha, Kamati ilibaini kwamba, hatua ya kutoshirikisha Kamati za Ulinzi na
Usalama za Wilaya ililenga kutovujisha siri dhidi ya watuhumiwa wa ujangili.
Hatua hiyo ilisababisha usumbufu mkubwa kwa viongozi wa mamlaka za utawala za
Wilaya na Mikoa kutokana na kulaumiwa na wananchi kwa kushindwa kuwasaidia pale
walipokumbwa na matatizo.
3.3 Mahojiano baina ya Kamati na Waheshimiwa Wabunge
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa suala hili liliibukia Bungeni baadaya wawakilishi wa
wananchi kupaza sauti kuhusu athari zilizowakumba wapiga kura wao, Kamati
iliona ni busara kuhoji baadhi ya Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja hii.
Wabunge hao walitoa taarifa muhimu kuhusu vitendo vilivyofanyika katika maeneo
yao wakati wa operesheni.
Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge walieleza kusikitishwa na namna ambavyo
Operesheni Tokomeza ilikiuka malengo yaliyokusudiwa na badala yake ikanyanyasa
wafugaji kwa kuangamiza mifugo yao na kuwaharibia mali zao kama vile; kuchoma
moto nyumba, kupora fedha na vitu vingine. Mbunge mmoja alinukuliwa katika
Taarifa Rasmi za Bunge akisema:-
“…badala ya Operesheni Tokomeza kusaka majangili, ikageuka kuwa Operesheni
Tokomeza Ufugaji…”
Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge waliieleza Kamati kuwa, siyo jambo la
kawaida kwa watu wanaoagizwa kufanya jambo fulani kwenda kinyume na maagizo.
Wakashauri kuwa, wahusika wote waliotenda kinyume namaagizo wachukuliwe hatua
stahiki ili kuepusha vitendo vya aina hiyo visijirudie katika operesheni
zitakazofuata. Pia Waheshimiwa Wabunge walishauri kasoro zilizojitokeza
zirekebishwe na operesheni iweze kuendelea ili kutowapa mwanya majangili
kujipanga upya.
3.3.1 Tathmini ya Kamati kuhusu majibu ya Waheshimiwa Wabunge Mheshimiwa Spika,
kimsingi Waheshimiwa Wabunge wanaunga mkono Operesheni Tokomeza ambayo ililenga
kukomesha vitendo vya kijangili na kunusuru raslimali za nchi hasa wanyamapori
na misitu. Hata hivyo, walieleza kusikitishwa na vitendo vilivyojitokeza wakati
wa utekelezaji wa operesheni na walisema haviwezi kuvumilika.
Mheshimiwa Spika, baada ya kupata taarifa mbalimbali kutoka kwa Waheshimiwa
Wabunge, mahojiano na viongozi na watendaji wa Wizara na kuzingatia taarifa
zilizowasilishwa na Serikali, Kamati iliazimia kuzuru baadhi ya maeneo
yaliyoathiriwa na Operesheni Tokomeza ili kufanya uhakiki.
4.0 KAMATI KUZURU MAENEO YALIYOATHIRIKA KWA AJILI YA KUHAKIKI
(VERIFICATION/OUTREACH)
Mheshimwa Spika, kutokana na wingi wa maeneo pamoja na ufinyu wa muda, Kamati
ilijigawa katika makundi matatu ili yaweze kutembelea baadhi ya maeneo yaliyoainishwa
katika Taarifa ya Serikali ili kufanya tathmini (verification) kwa utaratibu
ufuatao:-
4.1 Kundi la kwanza lilielekea Kanda ‘C’iliyohusisha maeneo yaliyoathiriwa na
Operesheni Tokomeza katika Mikoa ya Shinyanga, Kagera, Tabora, Kigoma, Rukwa,
Katavi na Singida.
Mheshimiwa Spika, kundi hili liliundwa na Wajumbe wafuatao:-
Mheshimiwa James Daudi Lembeli, Mb, Mheshimiwa Haji Khatibu Kai, Mb na
Mheshimiwa Susan Limbweni Kiwanga, Mb.
4.2 Kundi la pili lilielekea Kanda ‘B’iliyohusisha maeneo yaliyoathiriwa na
Operesheni Tokomeza katika Mikoa ya Simiyu, Mara, Arusha na Manyara.
Mheshimiwa Spika,kundi hili liliundwa na wajumbe wafuatao, Mheshimiwa
Abdulkarim E. Shah, Mb, Mheshimiwa Henry Daffa Shekifu, Mb na Mheshimiwa Amina
Andrew Clement, Mb.
4.3 Kundi la tatu lilielekea Kanda ‘D’iliyohusisha maeneo yaliyoathiriwa na
Operesheni Tokomeza katika Mikoa ya Pwani, Morogoro, Iringa, Ruvuma na Mtwara.
Mheshimiwa Spika, kundi hili liliundwa na wajumbe wafuatao; Mheshimiwa Kaika
Saning’o Telele, Mb, Mheshimiwa Muhammad Amour Chomboh, Mb na Mheshimiwa Dkt.
Mary Mwanjelwa, ambaye hata hivyo hakushiriki kutokana na dharura.
Mheshimiwa Spika,kama ilivyoainishwa hapo juu lengo la Kamati kutawanyika
Mikoani lilikuwa kutathmini athari zilizotokana na Operesheni Tokomeza ambayo
iliendeshwa nchini kuanzia tarehe 04 Oktoba, 2013 hadi tarehe 01 Novemba, 2013.
Mheshimiwa Spika, ili kutimiza jukumu hilo kikamilifu, Kamati iliongozwa na
taarifa zifuatazo;
i. Mpango Kazi wa Operesheni Maalum ya kupambana na Ujangili nchini,
ii. Taarifa ya Utekelezaji wa Operesheni Tokomeza iliyotolewa na Serikali.
iii. Michango ya Waheshimiwa Wabunge kama ilivyonukuliwa katika Taarifa Rasmi
za Bunge (Hansard).
iv. Madai yaliyotolewa na Wabunge kuhusiana na athari zilizotokana na
utekelezaji wa Operesheni Tokomeza.
v. Maelezo yaliyotolewa na Mashahidi ambao walihojiwa na Kamati.
vi. Vielelezo vilivyowasilishwa na Mashahidi waliofika mbele ya Kamati.
5.0 MAKUNDI YA KAMATI YALIVYOTEKELEZA MAJUKUMU YAKE
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza jukumu hili, Kamati ilikutanana makundi
yafuatayo:-
i. Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya
ii. Waheshimiwa Madiwani
iii. Waathirika wa Operesheni Tokomeza
5.1 Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya
Mheshimiwa Spika, Kamati ilikukutana na Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na
Wilaya na kupokea taarifa iliyohusu hali ya Ulinzi na Usalama hususan wakati wa
utekelezaji wa Operesheni Tokomeza.
Mheshimiwa Spika, kwa sehemu kubwa taarifa za Ulinzi na Usalama za Wilaya
zilisaidia kuanisha maeneo na matukio yaliyojiri wakati wa Operesheni Tokomeza
na athari zilizojitokeza. Wajumbe wa Kamati walitumia uchambuzi wa taarifa hizo
kupata uelewa zaidi kuhusiana na utekelezaji wa Operesheni hiyo kabla ya
kukutana na wananchi walioathirika ili kupata maelezo zaidi.
5.2 Waheshimiwa Madiwani
Mheshimiwa Spika,katika baadhi ya Wilaya, Kamati ilikutana nabaadhi ya Madiwani
wakiwa ni wawakilishi wa wananchi katika ngazi ya halmashauri ili kupata
maelezo zaidi kuhusu utekelezaji wa Operesheni Tokomeza kabla ya kukutanana
waathirika wa Operesheni.
5.3 Waathirika wa Operesheni Tokomeza
Mheshimiwa Spika, Kamati ilikutana nabaadhi ya wananchi walioathirika na
Operesheni Tokomeza na kupokea maelezo na malalamiko yao kuhusu namna
walivyoathiriwa na uekelezaji wa Operesheni.
Mheshimiwa Spika, wapo baadhi ya waathirika walitoa ushahidi/vielelezo vya
maandishi na picha ili kuthibitisha yale waliyokuwa wakiyaeleza mbele ya
Kamati. Wengine walikwenda mbali kiasi cha kuonesha majerahana makovu
waliyoyapata katika miili yao kutokana na mateso waliyopata kwenye kambi maalum
za mahojiano zilizoandaliwa na waendeshaji wa Operesheni Tokomeza.
5.4 Kuzuru maeneo yaliyoathirika zaidi na Operesheni
Mheshimiwa Spika, Kamati ilipata fursa ya kutembelea baadhi ya maeneo
yaliyokumbwa na athari za operesheni Tokomeza kwa lengo la kushuhudia mabaki ya
vielelezo ili kujiridhisha iwapo tuhuma za athari zilizotolewa kuhusu maeneo
hayo zilikuwa zakweli.
6.0 YALIYOBAINIKA KATIKA ZIARA ZA KAMATI
6.1 Vikao na Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa/Wilaya
Mheshimiwa Spika, katika vikaona Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa/
WilayaKamati ilibaini kuwa utekelezaji wa Operesheni Tokomeza haukushirikisha
viongozi wa maeneo hayo ya utawala.
Kulikuwa na manung’uniko kwamba licha ya Wakuu wa Wilaya na Mikoa kuwa
wawakilishi wa Rais, waliachwa kando na Operesheni kuendeshwa katika maeneo
wanayosimamia hadi malalamiko ya wananchi waliokamatwa yalipowafumbua macho
kwamba walikuwa wanateswa na kufanyiwa vitendo vya udhalilishaji na
watekelezaji wa Operesheni. Aidha,
Kamati ilielezwa kwamba utekelezaji wa Operesheni Tokomeza ulisababisha hofu
miongoni mwa wananchi na viongozi na kusababisha baadhi yao kukimbia makazi.
Mfano; Mkuu wa Wilaya ya Ulanga alikiri kujihifadhi kwenye Hoteli moja nje ya
Wilaya yake ambako alikutana na baadhi wananchi wake waliokimbia adha za
Operesheni Tokomeza.
Viongozi hao walieleza kwamba, kimsingi hawapingi Operesheni Tokomeza Majangili
kwaniililenga kunusuru raslimali za nchi hasa wanyamaporina misitu visitoweke
kutokana nakushamiri kwa vitendo vya ujangili. Hata hivyo, walieleza kuwa hatua
ya kutowashirikisha imelifanya zoezi hilo kuwa na kasoro nyingi pamoja na
udhalilishaji hata kwa viongozi waliochaguliwa na wananchi.
6.2 Vikao vya Kamati na Waathirika wa Operesheni Tokomeza
Mheshimiwa Spika, Kamati ilifanya mikutano mbalimbali katika baadhi ya maeneo
ilikofanyika Operesheni Tokomezakwa lengo la kuwasilikiliza waathirika na
kubaini mambo yafuatayo:-
Watuhumiwa kupekuliwa, kudhalilishwa na baadhi kutojulikana walipo
i. Mheshimiwa Spika, badhi ya wananchi wakiwemo viongozi, Madiwani na Wenyeviti
wa Vijiji na Vitongoji na Watumishi wa Serikali walikamatwa na kudhalilishwa
mbele ya wananchi wanaowaongoza. Baadhi ya watuhumiwa waliokamatwa walikuwa
hawajulikani walipo hadi Kamati ilipozuru maeneo hayo. Mfano; Vijana watatu wa
Kijiji cha Osteti, Kata ya Chapakazi, Wilayani Kiteto, walituhumiwa kujihusisha
na biashara ya Meno ya Tembo. Vijana hao ni Nyafuka Ng’onja, Ng’onja Kipana na
Mswaya Karani.
ii. Baadhi ya watuhumiwa waliokamatwa walidai kudhalilishwa mbele ya
wanafamilia kwa kupewa adhabu wakiwa uchi na wanawake kushikwa sehemu za siri
bila ridhaa yao. Mfano; ndugu Ali Nyenge (38) wa Kata ya Iputi, Wilaya ya
Ulanga alidai kuvuliwa nguo, kumwagiwa maji yaliyochanganywa na chumvi na kuchapwa
viboko huku mwanae wa kiume (11) akishuhudia.
Pia alidai kulazimishwa kuchora picha ya Chatu kwa kutumia wembe kwenye paja
lake. Vilevile, Bi. Neema Moses wa Babati alidai kuvuliwa nguo na kulazimishwa
afanye mapenzi na wakwe zake na pia kuingizwa chupa sehemu zake za siri.
Aidha, baadhi ya akina mama walidai kubakwa na kulawitiwa. Mfano; katika Kata
ya Iputi, Wilaya ya Ulanga, mwanamke mmoja alidai kubakwa na Askari wawili (2)
wa Operesheni Tokomeza Ujangili mida ya usiku. Vilevile, mama mmoja mkazi wa
Kata ya Matongo Wilayani Bariadi, alibakwa na askari watatu (3) wa Operesheni
Tokomeza Ujangili huku akiwa ameshikiwa mtutu wa bunduki
iii. Watuhumiwa waliokamatwa walifanyiwa upekuzi bila kuhusisha viongozi wa
Serikali za maeneo husika na kutokuwepo kwa mashahidi na hati za upekuzi.
Mfano; Ndg. Abdallah Pata naBi. Flora Mwarabu wa Kata ya Iputi Wilayani Ulanga
na Ndg. Elias Cosmas Kibuga wa Gallapo Babati, walipekuliwa bila kufuata
utaratibu.
Ukatili na Udhalilishaji katika Kambi za Mahojiano
iv. Mheshimiwa Spika, baadhi ya watuhumiwa waliopelekwa katika kambi za
mahojiano walidai kutwezwakwa adhabu zinazokiuka haki za binadamu. Mfano;
Diwani wa Kata ya Sakasaka wilaya ya Meatu Ndg. Peter Samwel, alidai kuadhibiwa
akiwa mtupu kwa kupewa adhabu za kijeshi kama kuning’inizwa kichwa chini miguu
juu, kupigwa kwa vyuma na kulazimishwa kufanya mapenzi na mti.
Mheshimiwa Spika, kutokana naukatili uliopitiliza, baadhi ya kambi za mahojiano
zilipewa majina kama vile Guantanamo (Ruaha), Goligota (Ngorongoro), Duma na
Andajega (Serengeti).
Upotevu wa mali za watuhumiwa na faini zisizoeleweka
v. Mheshimiwa Spika, ilidaiwa kuwa wakati wa utekelezaji wa Operesheni
TokomezaUjangili, baadhi ya watuhumiwa walipoteza mifugo, mali na fedha zao.
Mfano; katika Wilaya ya Ulanga Kata ya Iputimwananchimmoja alidai kuporwa
sanduku la VICOBA lenye shilingi laki saba na nusu (750,000/=) pamoja na simu
ya mkononi na Askari wa Operesheni Tokomeza waliovamia nyumbani kwake. Vilevile
Ndugu Musa Masanja wa Sakasaka Wilaya ya Meatu, alidai kuporwa shilingi laki
tatu 300,000/= pamoja na simu 2 za mkononi na Askari Askari wa Operesheni.
Mheshimiwa Spika,Pia ilidaiwa kuwa mifugo ya watuhumiwa ilikamatwa na kuingizwa
ndani ya maeneo ya hifadhina kufa kwa kupigwa risasi au kukosa maji na malisho
kutokana na kuzuiliwa kwa muda mrefu.
Baadhi ya mifugo ilitozwa faini bila stakabadhi au stakabadhi kuonesha viwango
vidogo ikilinganishwa na fedha halisi iliyolipwa. Mfano:Ndugu Sosoma Shimula
mwenye Ng’ombe 1700 Wilayani Kasulu alidai kwamba alitakiwa kulipa faini ya
shilingi Milioni thelathini (30,000,000/=, alipowasihi alipunguziwa hadi
Milioni kumi na mbili (12,000,000/=) hata hivyo aliweza kulipa Milioni kumi
(10,000,000/=).
Alionesha Kamati stakabadhi inayoonesha kuwa amelipa faini ya shilingi milioni
moja tu (1,000,000/=). Stakabadhi hiyo ilijazwa sehemu ya tarakimu, lakini
hakuna kilichoandikwa katika sehemu ya kiasi cha fedha kwa maneno. (Tazama
Kiambatisho Na. 4)
Watuhumiwa kuteswa na kuumizwa
vi. Mheshimiwa Spika, baadhi ya watuhumiwa walidai kupigwa na kuumizwa na
askari wa Operesheni na wengine kupata ulemavu wa kudumu. Mfano; katika Wilaya
ya Itilima,Kijiji cha Mbogo NdgSita Rumala alidai kupigwa na kuvunjwa mkono
alionesha wajumbe mkono uliokuwa umefungwa bandeji ngumu (P.O.P).
Aidha, Diwani Peter Samwel Ndekija wa Kata ya Sakasaka, Wilaya ya Meatu, alidai
kupigwa na kuumizwa vibaya mgongoni na alionesha kwa wajumbe wa Kamati makovu
aliyoyapata. Vilevile,ilielezwa kuwa Ndugu Munanka Machumbe (24) ambaye ni bubu
alipigwa risasi 3zilizomjeruhi mapajani na kuharibu sehemu za siri wakati
akijaribu kuwahoji Askari wa Operesheni kwa ishara sababu za kumtesa baba yake.
Aidha, katika tuko lingine Shekhe Mkuu wa Wilaya ya Ulanga Ali Mohamed (70)
aishiye kijiji cha Iputi, alidai kurushwa kichura na kutandikwabakora na Askari
wa Operesheni Tokomeza.Pia,Ndg. Nyasongo Magoro Serengeti waKata ya Majimoto
wilaya ya Mulele alidhalilishwa mbele ya wananchi wake. (Tazama Kiambatisho Na.
5)
Mifugo kuingizwa hifadhini nawatuhumiwa kubambikwa kesi
vii. Mheshimiwa Spika,wakati wa Operesheni, mifugo mingi ilikuwa
hifadhinilakini hata ile iliyokuwa nje ya hifadhi iliingizwa na askari wa
hifadhi na wafugaji kutakiwa walipe faini ya shilingi Milioni tatu
(3,000,000/=) hadi Sita (6,000,000/=) kwa idadi ya ng’ombe 30 hadi ng’ombe 100
na aliyeshindwa kulipa faini mifugo yake iliuawa au kupigwa mnada na mfugaji
kufilisiwa.
Walioshindwa kulipa faini mifugo ilipigwa mnada na wafugaji hawakuruhusiwa
kununua wala kukaribia eneo la mnada, na katika mnada mifugo iliuzwa kwa bei ya
chini kuliko faini iliyotozwa Mfano; shilingi elfu sitini (60,000/ kwa kila
ng’ombe.
Watuhumiwa kubambikwa kesi
viii.Ilidaiwa kwamba, baadhi ya watuhumiwa walidai kubambikwa makosa ambayo
hawahusiki nayo kama vile kumiliki silaha kinyume na sheria, kukutwa na bangi
au nyara za Serikalimfano; Bw. Elias Cosmas Kibuga wa Gallapo Babati alidai
kubambikiwa kesi ya kumiliki bunduki kukutwa na mkia wa twiga kinyume cha
sheria.
Mheshimiwa Spika, pia Bibi Zuhura Ali wa Kilombero alidai kuteswa huku akilazimishwa
kutoa silaha ambayo hakuwa nayo. Aidha, Bw. Melkzedeck Abraham Sarakikya wa
Itigi alidai kuteswa akilazimishwa atoe silaha.
Mateso na vifo kwa Watuhumiwa
ix. Mheshimiwa Spika, baadhi ya wananchiwalidai kuwa ndugu zao waliteswa
kikatili kwa muda mrefuna bila kupatiwa huduma za lazima kama chakula, maji na
matibabu (siku 1 -2) hadi mauti yalipowafika. Kwa mfanoNdg. Kipara Issa wa
Wilaya ya Kaliua na ndugu Emiliana Gasper Maro wa Gallapo, Wilaya ya Babati.
Aidha, wananchi hao walidaikuwa mahojiano kwa watuhumiwa yaliambatana na mateso
makali kwa muda mrefu kiasi cha kusababisha vifo. (Tazama Kiambatisho Na. 6).
Vilevile, watuhumiwa wengine waliodaiwa kupoteza maisha wakati wa Operesheni
Tokomeza ni Ndg. Wegesa Kirigiti wa Kijiji cha Remagwe na Ndg. Peter Masea wa
Kijiji cha Mrito (Tarime), Ndg. Mohamed Buto (Masasi) na Gervas Nzoya (Kasulu).
Mheshimiwa Spika, pamoja na uthibitisho wa picha zilizotolewa na wananchi
kuhusu kuteswa hadi kufa kwa Bi Emiliana Gasper Maro, Serikali kupitia
Mkurugenzi wa Wanyamapori ilitoa Taarifa kwa Umma ikipinga Taarifa iliyorushwa
na kituo cha luninga cha ITV tarehe 19 Oktoba 2013 kuhusu mauaji ya kutisha
yaliyofanywa na Askari wa kupambana na ujangili.
Taarifa hiyo ya Serikali inapinga kuwa Askari wa Operesheni Tokomeza hawauski
na kifo cha mtajwa. Taarifa hiyo imeonekana kukosa umakini kutokana na
kujichanganya juu ya watu inaowazungumzia. Taarifa hiyo inazungumzia majina
mawili tofauti (Evelyn Gasper na Mariana Gaspar Mallo wa eneo la Olongadiola)
wakati muathirika halisi ni Bi. Emilliana Gasper Maro wa Kijiji cha Orngadida,
Gallapo. (Tazama kiambatisho Na.7)
Ukatili dhidi ya Wanyama
x. Mheshimiwa Spika, kuhusu vitendo vya ukatili kwa wanyama ilidaiwa kwamba
ng’ombe walipigwa risasi, na ndama walikufa kwa kukosa maziwa kutokana na mama
zao kukamatwa na kuzuiwa kwenye mazizi yaliyopo maeneo ya hifadhi kwa muda
mrefu. (Tazama Kiambatisho Na.
Rushwa kwenye Mapori ya Akiba
xi. Mheshimiwa Spika,Wananchi walidai kukithiri kwa vitendo vya rushwa kwa
watumishi wanaosimamia mapori ya akiba ya Maswa, Kigosi Moyowosi, Burigi,
Kimisi na Mkungunero kwa kutaja majina ya baadhi ya watumishi wanaowatuhumu.
Mfano; Ndg. Kileo mtumishiwa pori la Maswa, alidaiwa kuwa na tabia ya kutoza
wananchi faini bila stakabadhi au kutoa stakabadhi kinyume na faini iliyotolewa
au kutoa stakabadhi bandia.
Aidha, katika pori la Kigosi-moyowosi, watumishi wafuatao walidaiwa kujihusisha
na vitendo vya rushwa; Ndg. Msocha, Alfred, Kobelo na Odhiambo.
Aidha, ilidaiwa kuwa katika mapori ya Kigosi Moyowosi na Kimisi zaidi ya
wafugaji 100 wenye ng’ombe wanaokadiriwa kuwa 50,000 wanalipia kuchungia
ng’ombe wao kwenye mapori hayo ya hifadhi tangu mwaka 2000 kwa malipo maalum na
hata Operesheni Tokomeza haikuwagusa.
Aidha, ilidaiwa kuwaNdg. Msocha (Meneja wa Pori la Akiba la Kigosi Muyowosi),
alituhumiwa na baadhi ya wananchi kuwa amekuwa akiwakodisha wafugaji hao kwa
vipindi vya miezi mitatu, na wafugaji huruhusiwa kulipa tena muda unapoisha.
Aidha, Mfugaji ambaye hulipa kiasi kidogo hulazimishwa kulipa huku akipigwa
namifugo yake kuuawa kwa kupigwa risasi.
Ilielezwa kuwa, Wafugaji na Askari Wanyamapori huwasiliana kwa simu ilil
kutekeleza makubaliano ya malipo kwa malisho yao. Nambaza simu zinazodaiwa kuwa
za Askari Wanyamapori zimeorodheshwa. (Tazama Kiambatisho Na. 9)
Mahusiano kati ya wananchi na Askari wa mapori ya Akiba
xii. Mheshimiwa Spika, wananchi wanaoishi kwenye Mapori ya Akiba yanayo
wazunguka walidai kuwa katika mahusiano mabaya naAskari wa mapori hayo.
Mfano;wananchi wa kijiji cha Kimotorok, Wilaya ya Simanjiro na Askari wa pori
la akiba la Mkungunero kiasi cha kufikia hatua ya kutishiana maisha. Vitendo
hivyo pia vipo kwa jamii zinazopakana na mapori ya Gurumeti.
Mahakama na Magereza kuzidiwa uwezo
xiii.Mheshimiwa Spika, kutokana na Operesheni Tokomeza ilidaiwa kuwa vyombo
Mahakama na Magereza katika maeneo husika vilizidiwa uwezo kutokana na wingi wa
kesi na idadi ya Mahabusu. Mfano;Gereza la Wilaya ya Bunda lenye uwezo wa
kuchukua jumla ya wafungwa na mahabusu 217 lililazimika kuchukua hadi watu 411.
Baadhi ya watuhumiwa waliokamatwa wanalazimika kusafiri umbali mrefu kuhudhuria
kesi zao. Mfano; katika wilaya ya Serengeti baadhi ya watuhumiwa walifunguliwa
kesi Wilaya za Tarime, Bunda na Bariadi.
Watumishi wa Umma kuhusishwa na Ujangili
xiv.Mheshimiwa Spika, ilidaiwa kuwa baadhi ya Watumishi waSerikali na vyombo
vya dola (Polisi) wanajihusisha na ujangili. Mfano niDereva wa OCD, Wilaya ya
Ngorongoro aliyetuhumiwa kujihusisha na ujangili wa Meno ya Tembo.
Askari huyo alihojiwa na viongozi wa Operesheni Tokomeza katika kituo chake cha
kazi. Vilevile, Ndg. Mohamed Ismail, Afisa Wanyamapori (W) Meatu anatuhumiwa
kukutwa na nyara zaSerikali.
Aidha,Askari Polisi wawili (2)Cpl. Isaack na PC Sixbert wa Mugumu Wilayani
Serengeti walikamatwa wakiwa na meno ya Tembo.
Mheshimiwa Spika, pia ilidaiwa kuwa baadhi ya Maofisa wa Serikali wamekuwa
wakitumia magari ya Umma ama kusafirisha au kusindikiza watoroshaji wa nyara za
Serikali. Mfano nigari la Serikali lililokamatwa likifaulisha meno ya Tembo
kutoka kwenye gari jingine huko Mkuranga kwa lengo la kuyasafirisha kwenda Dar
es Salaam.
Sambamba na hilo baadhi viongozi wa jeshi la Polisi wametuhumiwa kusaidia
watuhumiwa wa vitendo vya kijangili kutoroka na kuepuka mkono wa sheria.
Migogoro kuhusu mipaka ya Maeneo ya Hifadhi
xv. Mheshimiwa Spika,wananchi walidai kuwa baadhi ya Mapori ya Akiba naHifadhi
yamekuwa yakipanua mipaka yake bila kushirikisha wananchi wa maeneo
yanayowazunguka. Mfano; wananchi wa Wilaya ya Bunda wanaopakana na Pori la
Akiba la Gurumeti.
Pia, wananchi wa vijiji vya Kegonga na Masanga, katika Kata ya Nyanungu,
Wilayani Tarime wako katika mgogoro wa mpaka na TANAPA wakidai kuwa bonde la
Nyanungu limemezwa na eneo la Hifadhi kutokana na TANAPA kuongeza mipaka yake
bila kushirikisha wananchi wa maeneo hayo.
Aidha, katika Wilaya ya Ulanga kuna mgogoro katika kata za Iputi na Lupiro
dhidiHifadhi ya Selous.
Idara za Wanyamapori katika Halmashauri kukosa vitendea kazi
xvi.Mheshimiwa Spika, kutokana na silaha za Idara ya Wanyamapori katika baadhi
ya Halmashauri kuchukuliwa wakati wa Operesheni Tokomeza kwa ajili ya
uchunguzi, wananchi wamedai kupata shida kutokana na wanyama hasa Tembokuvamia
mashamba na kuharibu mazao pamoja na kujeruhi au kuua watu na mifugo.
Wanasiasa kushawishi wananchi kuishi kwenye maeneo ya Hifadhi
xvii. Mheshimiwa Spika, wakati wa kutekeleza Operesheni Tokomeza ilidaiwa kuwa
nyumba na maboma ndani ya mapori ya akiba zilichomwa moto. Mfano; Wilaya ya
Sumbawanga kijiji cha Msila Kata ya Mfinga na kijiji cha Kabage Wilaya ya
Mpanda. Hata hivyo baadhi ya wananchi wameanza kurejeakatika baadhi ya maeneo
ya hifadhi kutokana na ushawishi wa wanasiasa.
Mfano; katika Pori la Hifadhi ya Jamii Ubende Wilaya ya Mpanda walichangishwa
shilingi laki moja (100,000/ kwakila kaya kwa ajili ya kupatiwa huduma za
kisheria iwapo mamlaka husika zitajaribu kuwaondoa ndani ya hifadhi. Aidha,
Kamati ilipata taarifa kuwa, baadhi ya viongozi wa Vyama vya Siasa wamekuwa
wakigawa kadi za vyama vyao kwa wananchi wanaoishi katika maeneo ya hifadhi na kwa
ahadi kwamba, vyama walivyojiunga nga navyo vitawatetea wasiondoke katika
maeneo hayo.
Tatizo la Vibali vya Wakulima wa Muda
xviii. Mheshimiwa Spika, Kamati ilielezwa lipo tatizo la raia wa nchi jirani
kuingia nchini na kupewa vibali vyakuendesha shughuli za kilimo(Peasant
Permit)kwa muda, ambavyo hutolewa bilakubandika picha ya mhusika/mwombaji hasa
maeneo ya Karagwe.
Raia hao wanadaiwa kutumia nakala za vibali hivyo kuingiza nchini wahamiaji
haramu ambao baadhi yao huingiza makundi makubwa ya mifugo hasa ng’ombe na
wengine kutumia mwanya huo kuingiza silaha na kujihusisha na vitendo vya
ujangili katika baadhi ya mapori ya akiba. Mfano; Pori la Akiba la Ibanda
Rumanyika.
Vilevile kuna tatizo la majangili kutumia vivuli va wafugaji kuingia kwenye
hifadhi huku wakiwa wameficha silaha, na hivyo kuwepo mazingira ya kushindwa
kutofautisha kati ya majangili na wafugaji hususan katika maeneo ya hifadhi ya
Ruaha.
xix.Mheshimiwa Spika, kuna mgogoro katika eneo la Ushoroba (Buffer Zone) katika
Kata za Lupiro, Mbugana Iputi Wilaya ya Ulanga, maeneo ambayo jamii imejenga
miundombinu kwa miaka mingi ikiwa ni pamoja na shule, nyumba, mashamba,
misikiti na makanisa huku Serikali ikiwa kimya kwa muda mrefu.Hata hivyo,
wakati wa Operesheni Tokomeza wananchi hao walilazimishwa kuhama bila
kuelekezwa waende wapi.
Michango ya Waheshimiwa Wabunge kuhusu Operesheni
xx. Mheshimiwa Spika, Kamati ilibaini kuwa baadhi ya michango iliyotolewa na
Waheshimiwa Wabunge wakati wakichangia Hoja ya Mhe. Saidi Nkumba haikuwa
imefanyiwa utafiti wa kutosha kwani baadhi ya madai waliyoyatoa hayakuwa na
uhusiano na Oparesheni Tokomeza.
Kwa mfano;ni kweli kwamba ng’ombe 51 walitumbukia katika mto Rubana Wilayani
Bunda na kufa, hata hivyo tukio hilo lilitokea mwezi April, 2013 ikiwa ni miezi
6 kabla ya Operesheni. Aidha, ni kweli kuwa Wakazi wa Vijiji vya Kabage
Wilayani Mpanda na Luchima Wilayani Mulele walihamishwa kutoka katika maeneo ya
hifadhi na nyumba zao kuchomwa moto katika utaratibu uliofanywa na Halmashauri
hizo mwezi Septemba, 2013 kwa lengo la kuwapeleka kwenye maeneo rasmi ya
makazi.
7.0 MAONI NA USHAURI WA KAMATI KUHUSU TATHMINI YA UTEKELEZAJI WA OPERESHENI
TOKOMEZA
Mheshimiwa Spika, baada ya Kamati kuchambua nyaraka husika kuhusiana na
utekelezaji wa Operesheni Tokomeza, kuwahoji viongozi mbalimbali wa Wizara na
Waheshimiwa Wabunge, pamoja na kufanya ziara mikoani kwa lengo la kuhakiki
yaliyojiri kutokana na Operesheni Tokomeza, Kamati inapenda kutoa maoni na
ushauri ufuatao:-
i. Kwa kuwa, lengo la Operesheni Tokomeza lilikuwa kunusuru raslimali za nchi
hususani Wanyamapori na hasa Tembo na Misitu, na kwa kuwa Waheshimiwa Wabunge
na Wananchi wameiunga mkono mbali na matatizo ya kiutendaji yaliyojitokeza,
hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali irekebishe haraka kasoro zilizojitokeza
katika utekelezaji wa Operesheni Tokomeza ili kuendeleza na kukamilisha awamu
zote za operesheni kama zilivyo kwenye mpango na kunusuru raslimali za Taifa
hasa wanyamapori na misitu ambayo inatishiwa kutoweka kutokana na vitendo vya
ujangili.
ii. Kwa kuwa,Kamati imejiridhishakwamba matatizo na upungufu uliojitokeza
katika utekelezaji wa Operesheni Tokomeza yamechangiwa na maandalizi mabaya ya
Mpango kazi ambao Waziri Mwenye dhamana hakuidhinisha, na kwa kuwa,
imedhihirika kuwepo hali ya sintofahamu (kwa mujibu wa hansard) iliyosababishwa
na watendaji wakuu wa Wizara kwa makusudi kuamua kutomshirikisha kikamilifu
Waziri katika hatua za mwisho za maandalizi ya Mpango kazi, hivyo basi Bunge
linaazimia kwamba, Serikali iwachukulie hatua stahiki za kinidhamu Wasaidizi
Wakuu wote wa Waziri walioshiriki katika Mpango kazi huo.
iii. Kwa kuwa, Kamati imebaini kwamba pale Jeshi la Wananchi (JWTZ)
linaposhirikishwa katika Operesheni ufanisi mkubwa hupatikana, na kwa kuwa,
bado iko haja ya kuendeleza Operesheni Tokomeza kwa maslahi ya Taifa, na kwa
kuwa ushahidi wa mazingira ‘circumstantial evidence’ unaonesha kuwa Jeshi
lilichukua uongozi wa operesheni baada ya kugundua kuwa washiriki kutoka Vikosi
vingine (Polisi, TANAPA, TSF na NCAA) kwa kushirikiana na wafugaji wenye
ushawishi wa kifedha pamoja na wanasiasa, walihujumu operesheni hiyo kwa kutoa
taarifa kwenye mtandao mkubwa wa kijangili ambao umejengeka kuanzia Wizarani
hadi kwenye maeneo ya Hifadhi na kusaidia ‘majangili papa’ wasikamatwe, hivyo
basi, Bunge linaazimia kwamba:-
- Serikali kuchukua hatua za makusudi kuuvunja mtandao huo na pia;
- Kuandaa operesheni nyingine ambayo itapangwa na kutekelezwa na Jeshi la
Wananchi wa Tanzania na Idara ya Usalama wa Taifa.
iv. Kwa kuwa, kumekuwepo na operesheni kadhaa kabla ya Operesheni Tokomeza
ambazo zililenga kupambana na ujangili, na kwa kuwa, Operesheni Tokomeza
imeshindwa kupata mafanikio yaliyotarajiwa, na kwa kuwa, ushahidi wa mazingira
unaonesha wazi kwamba, Kikosi Dhidi ya Ujangili (KDU) kimeshindwa kutimiza
wajibu wake, hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali iimarishe kikosi
hicho kwa kukifanyia tathmini na kukiunda upya ikiwa ni pamoja na kukiwezesha
kwa rasilimali (Watu, fedha, magari, silaha za kisasa na vifaa vya mawasiliano
kama redio na simu).
Serikali iunde chombo ambacho kitakuwa na jukumu la kusimamia na kutathmini
utendaji kazi wa KDU. Iwapo utaratibu huo utazingatiwa ni wazi vitendo vya
ujangili vitadhibitiwa bila kutumia operesheni kubwa kama Uhai na Tokomeza.
v. Kwa kuwa, Kamati imebaini kuwepo kwa vitendo vya utesaji na ukatili wa hali
ya juu, ukiukwaji wa haki za binadamu na uzembe miongoni mwa Askari wa
Operesheni Tokomeza (ushahidi wa wahusika upo), hali ambayo imesababisha baadhi
ya Wananchi kupoteza maisha, kupata ulemavu wa kudumu pamoja na kupoteza mali
zao. Hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba:-
- Serikali Iwabaini wote waliohusika na vitendo vya kinyama, mateso na
udhalilishaji dhidi ya watuhumiwa, iwachukulie hatua stahiki na kuwasilisha
taarifa ya utekelezaji wa agizo hili katika Mkutano ujao wa Bunge.
- Ifanye tathmini ya kina kwa kupitia Wakuu wa Mikoa na Wilaya ili kujua athari
za Operesheni hii na kutafuta njia ya kutoa kifuta machozi kwa waathirika, ili
kurejesha imani ya Wananchi kwa Serikali yao.
vi. Kwa kuwa, Kamati imebaini kuwa Operesheni Tokomeza ilikuwa haikutengewa
fedha katika Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii katika mwaka wa fedha wa
2013/2014 na kwa kuwa kiasi cha fedha Tshs. 3,968,168,667/= kilichopatikana
kutoka Idara na Mashirika Tanzu ya Wizara haikutosheleza mahitaji ya fedha ya
Operesheni Tokomeza kutokana na ukubwa wa eneo la Operesheni, hivyo basi, Bunge
linaazimia kwamba, Serikali itenge Bajeti Maalum ya kutosheleza mahitaji ya
Operesheni Tokomeza.
Serikali kutenga Bajeti kwa ajili ya kuendeleza shughuli za uhifadhi katika
maeneo ya Hifadhi ikiwa ni pamoja na kuweka raslimali watu ya kutosha na
miundombinu mingine muhimu.
vii. Kwa kuwa, Kamati imebaini kuwa Taarifa kwa Umma iliyotolewa kwa Vyombo vya
Habari na Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori tarehe 23 Oktoba 2013, haikuwa
sahihi na pia ililenga kuudanganya Umma kwa kuficha mazingira na sababu za kifo
cha Bi Emilliana Gasper Maro, hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali
ichukue hatua za kumwajibisha Mkurugenzi wa Idara ya Wanyapori kwa kuudanganya
umma kwa kujaribu kuficha ukweli.
viii.Kwa kuwa, Kamati imebaini kuwa kumekuwapo mchezo mchafu unaofanywa na
baadhi ya Maafisa Wanyamapori, Maafisa Misitu katika mapori ya akiba, Misitu ya
Serikali na katika baadhi ya Hifadhi za Taifa wa kupokea rushwa, kutesa
wananchi, kuwabambika kesi na kujihusisha na ujangili,na kwa kuwa Kamati inayo
majina na vielelezo vya wahusika, hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali
ifanye tathmini nchi nzima kwa lengo la kutambua kiwango cha vitendo vya rushwa
miongoni mwa watumishi hao, na kuwachukulia hatua stahiki za kinidhamu wale
watakaobainika kuhusika ikiwa ni pamoja na kuwawajibisha na kuwafikisha kwenye
vyombo vya sheria.
ix. Kwa kuwa, Kamati imebaini kuwa baadhi ya viongozi wa kisiasa na Serikali waliingilia
utekelezaji wa Operesheni Tokomeza kwa manufaa yao binafsi, kwa mfano, agizo la
kuwataka wahusika wa Operesheni Tokomeza kutowagusa Viongozi wa Kisiasa wa
ngazi zote, kauli ambayo ilitafsiriwa kuathiri utekelezaji wa Operesheni
Tokomeza kwa kubagua Watanzania katika makundi ya Viongozi na Wananchi wa
kawaida, hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali ihakikishe kuna
uwajibikaji wa pamoja pale inapoamua kutekeleza jambo la Kitaifa kama
Operesheni Tokomeza.
x. Kwa kuwa, Kamati imethibitisha kuwa, baadhi ya wanasiasa wamekuwa
wanawadanganya wananchi waliothibitika kufanya shughuli za uchumi kwenye maeneo
ya hifadhi, na kuwaahidi kuwatetea pindi Serikali inapochukua hatua za
kuwaondoa katika sehemu hizo, ikiwa ni pamoja na kuwapa kadi za vyama vyao vya
siasa, hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba, serikali ihakikishe kwamba,
wananchi hawaendeshi shughuli za kiuchumi kwenye maeneo ya hifadhi na kuwaonya
wanasiasa waache kuwalaghai wananchi kwa maslahi yao binafsi.
xi. Kwa kuwa,Kamati imebaini kwamba katika baadhi ya maeneo ya mipakani mfano
Karagwe, Idara ya Uhamiaji hutoa vibali kwa raia wa nchi jirani vya kuishi na
kulima hapa nchini, vibali ambavyo havina udhibiti wala tija kwa nchi, na
kusababisha migogoro ya mara kwa mara kati ya wakulima na wafugaji lakini pia
uharibifu wa mazingira kwa kuingiza mifugo hifadhini, hivyo basi, Bunge
linaazimia kwamba, Serikali isitishe mara moja zoezi la kutoa vibali hivyo,
kufuta vilivyopo na kuwataka raia hao wa kigeni wenye vibali kuondoka Nchini
mara moja.
xii.Kwa kuwa, Kamati imebaini kwamba zaidi ya asilimia 25 ya eneo la Nchi ni
hifadhi, namipaka ya maeneo mengi yaliyohifadhiwa haijaainishwa, na kwa kuwa
Serikali haina uwezo wa (raslimali watu na fedha) wa kusimamia na kulinda
mipaka ya maeneo haya kikamilifu, hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali
kufanya yafuatayo:-
• Kuridhia Idara ya Wanyamapori na Wakala wa Huduma ya Misitu kuajiri idadi ya
watumishi wanaotakiwa kama Serikali bado inaendelea kuyahifadhi maeno hayo.
• Kuainisha mipaka ya mapori yote ya akiba, hifadhi za taifa na Misitu ya
Serikali kwa alama maalumu na za kudumu ili kuepusha Wananchi kuingia katika
maeneo hayo kwa kutojua mipaka.
• Kuyaachia mapori ya Serikali ambayo yamekosa sifa, ili yatumike kwa kilimo na
ufugaji kwa kuzingatia mpango wa matumizi bora ya ardhi.
xiii.Kwa kuwa,yapo maeneo ya mapori na Hifadhi ambayo yana migogoro ya muda
mrefu ambapo wananchi wameishi katika maeneo hayo kwa muda mrefu, hivyo basi,
Bunge linaazimia kwamba, Serikali irekebishe mipaka husika au iwahamishie
Wananchi hao kwenye maeneo mengine yenye miundombinu. Serikali iwaagize
Mawaziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Maliasili na Utalii na Tawala
za Mikoa na Serikali za Mitaa kutembelea maeneo yote yenye migogoro nchini na
kuitafutia ufumbuzi ili wananchi waweze kuelewa hatma yao katika maeneo hayo
kwani wamekuwa katika hali ya sintofahamu kwa muda mrefu.
xiv.Kwa kuwa, Kamati imebaini kuwepo kwa migogoro baina ya Wananchi, Wawekezaji
na hifadhi katika maeneo ya Meatu, Tarime, Bunda na ile ya Loliondo na
Kimotorok ambayo inashughulikiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, hivyo basi, Bunge
linaazimia kwamba, Serikali ihakikishe inamaliza (kama ilivyoahidi) migogoro
iliyopo Loliondo na Kimotorok na maeneo mengine mapema iwezekanavyo.
Kurekebisha haraka kasoro zote za kisheria zilizokiukwa kwa makusudi na Idara
ya Wanyamapori kiasi cha kusababisha mgogoro baina ya Halmashauri ya Wilaya ya
Meatu na mwekezaji katika Pori la Hifadhi ya Jamii la Makao pamoja na
kuwawajibisha Watendaji wa Idara ya Wanyamapori waliosababisha mgogoro huo.
xv.Kwa kuwa, Kamati imebaini kwamba, migogoro wanayokumbana nayo wafugaji
kutokana na kuingiza mifugo kwenye maeneo ya hifadhi pamoja na kero nyingine ni
kutokana na kukosekana kwa miundombinu sahihi na endelevu kwa ajili ya ustawi
wa mifugo, na kwa kuwa, Mheshimiwa Rais aliunda Wizara mahsusi kwa ajili ya
kuendeleza Sekta ya Mifugo nchini akitambua umuhimu wa Sekta hii kwa uchumi wa
Taifa, na kwa kuwa, Tanzania ni ya pili kwa wingi wa mifugo Barani Afrika, ni
wazi kwamba adha wanazokumbana nazo wafugaji ni matokeo ya kutokuwepo sera na
mipango madhubuti ya muda mfupi na mrefu.
Hivyo basi, Bunge linaishauri Serikali kumtaka Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na
Uvuvi, kujipima na kuona iwapo bado anastahili kuendelea kuhodhi wadhifa alionao.
xvi.Kwa kuwa, Kamati imebaini kuwa baadhi ya madai yaliyotolewa na Waheshimiwa
Wabunge Bungeni wakati wakichangia Hoja ya Mhe. Saidi Nkumba ilikuwa ni ya
kweli; na kwa kuwa yaliyoelezwa katika madai hayo hayana uhusiano na Operesheni
Tokomeza kwani yalitokea kabla ya Operesheni hiyo; hivyo basi, Bunge linaazimia
kwamba, Waheshimiwa Wabunge kuwa makini zaidi na kufanya utafiti kwa lengo la
kuhakikisha michango yao inakuwa sahihi na inalenga hoja mahsusi iliyo mbele ya
Bunge.
8.0 HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, jukumu uliloikabidhi Kamati hii lilikuwa zito na lilihitaji
umakini mkubwa na muda wa kutosha katika kulitekeleza. Kutokana na ufinyu wa
muda na mazingira magumu wakati wa kutekeleza jukumu hilo, Kamati inakiri
kwamba haikuweza kutembelea maeneo yote yaliyoathirika na zipo lawama kutoka
kwa baadhi ya wananchi kwamba, Kamati haikuweza kupita katika maeneo yao.
Mheshimiwa Spika, Kamati inapenda kuwahakikishia wananchi wote kuwa, kupitia
taarifa mbalimbali za viongozi na wawakilisihi wa waathirika mbele ya Kamati,
malalamiko yao yamezingatiwa na kufanyiwa kazi.
Mheshimiwa Spika,kama tulivyoeleza katika maelezo yetu ya utangulizi, Kamati
inaamini na kote tulikopita wananchi wanakiri kuwa, lengo na azma ya Serikali
kuanzisha Operesheni Tokomeza Ujangili lilikuwa jema kwani lililenga kunusuru
maliasili zetu kwa ajili ya maendeleo endelevu na heshima ya Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, Kamati inaamini maelezo yote yaliyotolewa na wananchi pamoja
na viongozi wao yalikuwa na dhamira njema. Aidha, mapendekezo yaliyotolewa na
Kamati yanalenga kuisaidia Serikali kuchukua hatua za makusudi na haraka
kurekebisha kasoro zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wa Operesheni Tokomeza
Ujangili, ili kuepuka kutokea kwa vitendo vinavyoashiria ukiukwaji wa misingi
ya haki za binadamu na Utawala Bora nchini.
Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe binafsi kwa dhati kutokana na
kuiamini Kamati yangu na kuikabidhi jukumu hili zito. Hii ni ishara tosha
kwamba una imani na Wabunge wako na kwamba wanaweza kufanya kazi kwa niaba
yako.
Mheshimiwa Spika, pia nitoe shukrani za dhati kwa Katibu wa Bunge, Dkt. Thomas
Didimu Kashilillah, kwa kuiwezesha Kamati hii kufanya kazi yake vizuri na
kuikamilisha kwa wakati. Aidha, kwa namna ya pekee napenda kuwashukuru makatibu
walioihudumia Kamati hii wakiongozwa na Ndugu Theonest K. Ruhilabake ambao ni
Ndugu Gerald Magili, Ndugu Chacha Nyakega na Ndugu Stanslaus Kagisa.
Aidha, ninapenda kuwashukuru viongozi wa Mikoa, Wilaya, Kata na Vijiji ambao
walionyesha ushirikiano mkubwa Kamati ilipotembelea maeneo yao.
Mheshimiwa Spika, mwisho lakini si kwa umuhimu Kamati inawashukuru watumishi
wafuatao; Ndugu Silva Chindandi, Ndugu Ndigwako Mwaigaga, Ndugu Victoria
Mizengo, Ndugu Germina Magohe na watumishi wengine ambao kwa namna moja au
nyingine walishiriki katika kuihudumia Kamati hii hadi inakamilisha taarifa
hii.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
James Daud Lembeli, Mb
MWENYEKITI KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA ARDHI, MALIASILI NA MAZINGIRA